Uchambuzi Viwanja bora huongeza ubora wa Ligi Kuu

 Wachezaji wa Mbeya City wakishangilia baada ya kuifunga Prisons kwenye Uwanja wa Sokoine ambao ni kati ya viwanja vilivyofungiwa. Picha na maktaba. 
  • Viwanja vilivyofungiwa ni Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi wa Tabora, Uwanja wa Jamhuri wa Dodoma, Uwanja wa Sokoine wa Mbeya, Sheikh Amri Abeid wa Arusha, Kaitaba wa Bukoba, Mkwakwani wa Tanga na Majimaji wa Songea.
SHARE THIS STORY
0
S
  • Viwanja sita vyafungwa Ligi Kuu

BODI ya Ligi  Tanzania Bara (TPL)  imevifungia viwanja saba vinavyotumika kwa ajili ya Ligi Kuu  na Ligi Daraja la Kwanza Tanzania  Bara msimu huu.
Viwanja vilivyofungiwa ni Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi wa Tabora, Uwanja wa Jamhuri wa Dodoma, Uwanja wa Sokoine wa Mbeya, Sheikh Amri Abeid wa Arusha, Kaitaba wa Bukoba, Mkwakwani wa Tanga na Majimaji wa Songea.
TPL imevifungia viwanja hivyo kutokana na matatizo mbalimbali yakiwemo ya mapaa, majukwaa, sehemu ya vyumba vya kubadilishia nguo na eneo la kucheza mpira wa miguu.
Bodi ya Ligi imechukua hatua hiyo wakati Ligi Kuu Bara imesimama hadi mwishoni mwa Januari kwa hiyo kuna kipindi kirefu hadi vitumike kwa ligi hiyo.
Ni matarajio yetu kwamba wamiliki wa viwanja hivyo watachukua hatua thabiti katika kuvifanyia matengenezo viwanja vyao ili viwe kwenye hali nzuri kabla ya mashindano hayo kuanza tena.
Ieleweke kwamba hakuna maendeleo ya mpira wa miguu kama kutakuwa hakuna viwanja bora vya kuchezea kwani juhudi zote zingine zitakazofanywa hazitazaa matunda.
Viwanja ni moja ya nyenzo muhimu katika mpira wa miguu kwa hiyo ni muhimu kwa kila mdau kuelewa jambo hilo na wanaohusika kulitilia mkazo kwa kuwa na viwanja bora.
Inafurahisha pia kusikia kwamba Shirikisho la Soka la Tanzania (TFF) linaunga mkono hatua ya Bodi ya Ligi kuwa litaisaidia ili kuhakikisha kuwa mpira wa miguu unachezwa katika viwanja bora.
Lakini, ni  muhimu sana kwa TFF na Bodi ya Ligi kuhakikishwa kwamba viwanja ambavyo havikufanyiwa marekebisho yanayotakiwa havitumiki katika mzunguko wa pili wa ligi hizo.
Klabu za Tanzania zinapaswa kuwa na viwanja vyake, lakini ukweli ni kwamba baadhi ya klabu hizo hazina uwezo wa kumiliki au kujenga viwanja kwa ajili yao. Lakini, ziko klabu zenye uwezo wa kuwa na viwanja kama vile Simba na Yanga kutokana na rasilimali kubwa waliyonayo ikiwemo wingi wa wanachama na mashabiki wanaoziunga mkono.
Kwa hiyo, wakati umefika kwa klabu za Simba na Yanga kuwa na viwanja vya kisasa ambavyo watavitumia kwa kucheza mechi za nyumbani za Ligi Kuu na mechi za kirafiki.
Jambo hilo mbali na kuwapunguzia gharama za michezo pia zitawaongezea kipato na katika uwanja huo wanaweza kutoa ofisi na sehemu za kufanyia biashara ambazo zitawaingizia fedha nyingi.
Klabu za Simba na Yanga zina nafasi ya kuingia ubia na kampuni kadhaa zikiwemo benki katika mradi wa ujenzi wa uwanja wa kisasa ambao utakuwa ni kitega uchumi kikubwa.
Viongozi wa klabu hizo wanatakiwa kufungua macho na kuziona fursa za maendeleo ya klabu zao na kuzichangamkia badala ya kuziendesha klabu hizo kwa mtindo wa kizamani wa kutegemea mapato ya mlangoni tu.
Mapato ya mlangoni ni muhimu lakini yakiongezeka na vyanzo vingine vya mapato vitavijengea klabu hizo kuwa na uwezo mkubwa wa kifedha na kuwa na uwezo wa kusajili wachezaji bora zaidi na wakati huo wataanza kuwa na wazo la kuchukua ubingwa wa Afrika. Hakuna sababu yoyote ile kwa sasa ambayo inazifanya Simba na Yanga na hata Azam za Dar es Salaam kuwa zisiwe klabu kubwa na zinagombania vikombe vya Afrika kwenye hatua za fainali kila mwaka.

No comments:

Post a Comment